Skip to main content

Namna ya Kuandaa Kitalu cha Miche


Utangulizi
Kitalu ni sehemu maalumu iliyopangiliwa kwa ajili ya kutunzia miche michanga kabla ya kuipeleka shambani ama bustanini. Sio mimea yote inahitaji vitalu ila mimea mingi inahitaji vitalu. Mimea kama mahindi, maharage, karoti, kunde na mchicha haihitaji vitalu. Mimea kama kabeji, vitunguu, sukuma wiki, chainizi, nyanya, bilinganya, hoho, matikiti, matango na mengineyo huhitaji kitalu. Pia miti mingi ya matunda, kuhifadhi mazingira, mbao, dawa nakadhalika huhitaji kitalu. Mimea ambayo inasumbua kupandikiza na ambayo inachipua haraka inashauriwa kupandwa moja kwa moja shambani ambapo haitasumbuliwa kuhamishwa. Mimea ambayo inachelewa kuchipua, kukua, na yenye kuhitaji matunzo au kuhudumiwa kwa karibu wakati ikiwa michanga inashauriwa ipandwe kwanza kwenye kitalu hadi itakapopata miche inayotakiwa kisha kupandikizwa bustanini au shambani.

Aina za vitalu
  1. Vitalu vya kawaida vya matuta 
  2. Vitalu vya vimfuko (viriba)
  3. Vitalu vya boksi
Namna ya kuchanganya na upandaji
Weka udongo debe mbili, mbolea debe moja na makapi ya mpunga ama mchanga debe moja. Changanya vizuri kwa kutumia koleo na utandaze huo mchanganyiko kwa kutumiaa reki. Panda au sia mbegu bora ambazo zimekomaa na kukauka vizuri, ambazo hazijashambuliwa na magonjwa au wadudu na zenye uwezo wa kuota vizuri zikipandwa. Kama unahitaji kununua mbegu inashauriwa kununua mbegu kutoka kwa mawakala wanaoaminika. Unaweza kupanda kwa mstari ama kwa kusia. Miche ikiwa tayari ikapandwe bustanini wakati wa jioni na imwagiliwe vizuri. Bustani iwe imeandaliwa kabla ya siku ya kuhamisha miche. Udongo kwenye kitalu unatakiwa uwe unaweza kupitisha maji vizuri. Tayarisha kitalu chako kwa kuchimba au kulima udongo angalau 30 sm kwenda chini, ondoa mabaki yoyote ya mimea na mizizi na vunja mabonge yote ya udongo kisha changanya samadi iliyooza vizuri au mboji iliyoiva vizuri. Sawazisha vizuri na reki hadi udongo uwe vizuri.
Pima upana na urefu wa kitalu ambao utakuwezesha kufikia kila pembe ya kitalu kwa urahisi bila kukanyaga ndani ya kitalu. Hii itasaidia kupunguza uwezekano wa kuleta magonjwa kwenye kitalu na itarahisisha kungoa magugu pamoja na kuhamisha miche kwenda shambani. Kama unasia mbegu katika mistari hakikisha kuwa mistari ipo katika umbali wa sm 7-10. Baada ya kusia mbegu funikia na udongo kidogo kutegemea na ukubwa wa mbegu. Siku moja kabla ya kusia mbegu, mwagia kitalu maji hadi kilowe vizuri. Kwa siku zinazofuata inashauriwa kumwagilia maji kidogo kidogo hadi pale zitakapochipua.

Namna ya kutayarisha kitalu
Mahitaji
  • Makapi ya Mpunga
  • Debe
  • Mbolea samadi au mboji
  • Jembe  au Koleo
  • Udongo
  • Maji na Reki
Sifa za sehemu nzuri ya kutengeneza kitalu
  • Karibu na chanzo cha maji au bomba.
  • Sio mbali na shambani/bustanini.
  • Mbali na wanyama ama kuwe na uzio.
  • Pasiwe na upepo mkali
  • Iwe na kivuli.
  • Iwe karibu na njia kurahisisha usafirishaji pindi ikibidi.
Matunzo ya kitalu
Baada ya kusia mbegu hakikisha kitalu hakipati jua la moja kwa moja na mvua kubwa. Weka matandazo ya majani ili kusaidia udongo kuhifadhi unyevunyevu na kuweza kuzuia mwangaza wa jua wa moja kwa moja.
Angalizo:
  • Ondoa matandazo mara tu mbegu zitakapochipua
  • Ruhusu kivuli kidogo kwenye miche na usiweke kivuli kikubwa sana kwani kitaifaya miche isikue
  • Baada ya kuchipua mwagilia maji taratibu kwa kutumia bomba au chupa yenye vitundu vidogo dogo.
  • Hakikisha maji hayazidi kwenye kitalu kwani yanaweza kusababisha ugonjwa na miche kuharibika.
  • Hakikisha kitalu ni kisafi wakati wote. Ondoa magugu yoyote yatakayojitokeza.
  • Punguzia miche kama imejazana sana ili kuipa nafasi ya kukua vizuri.
  • Kagua kitalu mara kwa mara kuangalia kama kuna uvamizi wowote wa wadudu waharibifu au mlipuko wa ugonjwa.
Baada ya miche yako kufikia muda wa kupandikiza inashauriwa kuchagua miche yenye afya nzuri ambayo haijaathirika na wadudu wala kuwa na dalili yoyote ya ugonjwa. Mwagilia maji kwenye kitalu usiku mmoja kabla ya siku ya kung’oa ili kurahisiha ung’oaji na kuzuia uwezekano wa mizizi kuharibika. Hakikisha miche iliyong’olewa haipati jua la moja kwa moja au hewa yenye joto. Inashauriwa kuiweka kwenye trei au kikapu na kuifunika na majani au nguo mbichi wakati inapelekwa shambani au bustanini.

Namna ya kupandikiza miche kwenye Shambani/Bustanini
  • Panga kupandikiza miche shambani au bustanini siku ambayo jua siyo kali sana au wakati wa jioni wakati jua linakaribia kuzama.
  • Manyunyu ya mvua ni muhimu na husaidia sana wakati wa kupandikiza.
  • Shindilia udongo vizuri kuzunguka mizizi ya mche kwa kutumia vidole vyako ili kuufanya mche ujishike vizuri kwenye udongo.
  • Hakikisha unaweka nafasi ya kutosha kati ya mmea na mmea na mstari hadi mstari ili kuacha nafasi ya mizizi kutanukia na majani kuchanulia hapo baadaye.
  • Kama hamna mvua wakati wa kupandikiza inashauriwa kumwagilia hata kama mimea haionyeshi dalili za kukauka.
  • Ikinge mimea iliyopandikizwa na jua la moja kwa moja hadi wakati ambapo itaonyesha kuwa imeshika kwenye udongo, inaweza kukua yenyewe na kuhimili mwanga wa jua.
Faida za Kitalu cha miche kwa mkulima
  • Kuchagua miche iliyo na afya nzuri.
  • Kuthibiti magugu shambani kabla hajahamishia miche shambani.
  • Kupata miche ya kupanda muda wowote atakao.
  • Ni rahisi kuthibiti vijidudu viharibifu na magonjwa kwenye kitalu kuliko shambani ama bustanini. Hii ni kwa sababu kitalu kinakua na miche mingi na huchukua nafasi kidogo.
  • Ni rahisi kuhudumia miche iliyo kwenye kitalu kuliko bustanini.
  • Kuweza kuuza miche kwa wakulima wengine.

Comments

Popular posts from this blog

Utengenezaji wa Chakula cha Kuku wa Nyama (Bloilers)

Utangulizi Kuku wa nyama wana mahitaji yafuatayo ya viinilishe katika chakula ili wakue vizuri Viinilisha vya wanga 60-65%   Protini 30-35%   Madini 2-8% Chakula cha Vifaranga Chakula hiki hutengenezwa katika namna ya kumsaidia kifaranga aweze kumeza vizuri na hivyo hakitakiwi kuwa katika punje punje. Hata kama utanunua pumba, ni vema kuzipitisha kwenye mashine ili ziwe laini zaidi.  Mahitaji (kgs)  Unga wa dona wa nafaka kama mahindi au mtama 40  Pumba za mtama au mahindi au uwele 27  Mashudu ya alizeti au ufuta, au pamba au karanga n.k. 20  Unga wa mifupa au chokaa ya kuku (DCP) 2.25  Dagaa au mabaki ya samaki (sangara fish meal) 10  Chumvi ya jikoni 0.5  Virutubisho (Broiler premix) 0.25  Jumla utapata 100Kg. Chakula cha kukuzia – growers mash Mahitaji (Kg) Mahindi yaliyobarazwa au mtama au uwele 25   Pumba za mtama au mahindi au uwele 44   Mashudu ya alizeti au ufuta, au pamba au karanga n.k. 17   Unga wa mifupa au chokaa ya kuku (DCP) 3.25   Dagaa au mabaki ya samaki (fish meal) 1

Aina Za Miti ya Minazi

AINA ZA MINAZI Inafaa mkulima kufahamu kuna aina mbali mbali za minazi na ina mahitaji tofauti katika ukuaji. Ujuzi huu utamsaidia katika kuchagua aina ya minazi itakayofaa kwa eneo lake na kwa kiwango chake cha utunzaji. KUNA AINA TATU ZA MINAZI Minazi mirefu ya asili Minazi mifupi Minazi chotara MINAZI MIREFU YA ASILI (EAT) Minazi ya aina hii ndiyo inayojulikana na wakulima wengi kwa vile ni ya kiasili na imezoea mazingira yetu. Minazi hii huchukua miaka 6-8 tangu kupandikizwa hadi kuzaa. Minazi ya aina hii huvumilia ukame na inao uwezo wa kutoa wastani wa nazi 40 kwa mwaka. Nazi huwa kubwa na zenye nyama nene ambayo inafaa kwa kupikia na kukamua mafuta. Minazi hii huishi kad ya miaka 60 na kuendelea. Nchini Tanzania, minazi hii hustawi vyema ukanda wa pwani sehemu zisizo na mawe na ambazo hazituamishi maji. MINAZI MIFUPI (DWARF) Minazi ya aina hii huzaa mapema kuanzia miaka miwili. Huzaa nazi nyingi na ndogo. Nazi hizi huwa na nyama nyembamba hivyo hutumika kwa nnadafu. Minazi huhit

Kilimo cha Miti ya Mbao - Uwekezaji wa Muda wa Kati na Mrefu

Utangulizi Kilimo cha miti ni uwekezaji wa muda wa kati na mrefu (mid & long term investments). Ila kwa kawaida jamii nyingi hasa za kiafrika huwa hazivutiwi na uwekezaji wa muda mrefu. Hata hivyo kama una mpango wa kuwa imara kiuchumi inashauriwaau yakupasa kufikiria na kujifunza aina za uwekezaji wa muda mrefu. Miti hutumika kwa matumizi mengi mfano mbao, nguzo za umeme na kujengea, mapambo, kuni na mkaa, kuzalisha matunda, mitishamba na madawa,  utengenezeaji wa karatasi n.k.  Mchanganuo Ekari moja ya shamba unaweza kupanda miti mia sita (500) mpaka mia saba (700). Gharama za kununua mashamba au maeneo ya kupandia miti hutegemea na eneo. Kwa  sehemu nyingi za vijijini maeneo kwa ekari moja hayazidi laki 5.  Miche ya kununua mfano Mitiki huuzwa kuanzia elfu moja (1000) kwa mche mmoja Gharama ya kununua miche =  1000 * 600 = 600,000   Pia unaweza kuokoa gharama za kununua miche kwa kuioteshe mwenyewe ktk vitalu na kuiamishia shambani baada ya kustawi vizuri na kuwa imara.  Mf. Mbe